Games

LATEST UPDATES
Showing posts with label kitaifa. Show all posts
Showing posts with label kitaifa. Show all posts

Thursday, March 24, 2016

VISASI VYA MAGUFULI VYAWACHOSA WASOMI, WAMPONDA

RAIS John Magufuli anatajwa kuwa ni rais mchochezi na anayefanya mambo yake ili kuonesha anaendesha mapambano dhidi ya wapinzani wake, 

Na Happyness Lidwino.

Dk. Azaveli Lwaitama, Mhadhiri Mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam amesema, yapo baadhi ya mambo ambayo Rais Magufuli amekuwa akiyafanya ili kukomoa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

“Mfano siku aliyoteuliwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda aliongea kauli tata akaendelea na kauli hizo tata.

“Kuteuliwa kwa Makonda inatafsiri mpambano utakaokuwepo baina ya Meya mpya na yeye (Makonda) kwa kuwa, wanaoteuliwa na rais siku zote huwa wanajiona kuwa juu,” amesema Dk. Lwaitama.

“Hata Makonda nimemuacha Dar es Salaam ili wabaya wake wamuone akipanda cheo, wenye chuki wajinyonge zaidi,” amenukuliwa Rais Magufuli wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa kituo cha kufua umeme cha Kinyerezi namba mbili.
Amesema Dk. Lwaitama, Rais Magufuli anatakiwa kufanya kazi bila upendeleo kwa kuwa lengo ni kuwatumikia wananchi na si vinginevyo.
Dk. Lwaitama anasema hayo wakati Chama Cha Mapinduzi (CCM) kikilitumbikiza taifa kwenye sintofahamu ya kisiasa na kwamba, ni wakati wa wananchi kukataa utumwa,
Dk. Lwaitama anasema, wananachi wanapaswa kuondoka kwenye minyororo ya utumwa na kusimama katika kuhakikisha wanapigania haki pale inapoonekana kupokwa na watawala.
Anatoleo mfano ushindi wa vyama vinavyoundwana ukawa kuchukua Umeya wa Jiji la Dar es Salaam ambapo ndio Mji Mkuu wa Kibiashara Tanzania na kwamba, hatua hiyo inaanza kufungua minyororo.
“Wananchi wanatakiwa kujiandaa kimabadiliko na kuukataa utumwa kwani kwa muda mrefu walikuwa utumwani kwa kuongozwa na chama kimoja,” anasema Dk. Lwaitama.
Anasema, wananchi wa Dar es Salaam amekuwa wakijiuliza sababu za kughairishwa uchaguzi huo mara kwa mara “yote hii ni kwa sababu CCM inang’ang’ania madaraka.”
Akizungumza na mtandao huu leo Dk. Lwaitama anasema jeuri ya watawala wa nchi hii inatokana na ubovu wa Katiba na kwamba, udhaifu huo unakwenda mbali ikiwa ni pamoja na kuteua viongozi wabovu.
Miongoni mwa viongozi anaowaona kutokuwa na mantiki ya kuwepo kwao licha ya rais kuwa na mamlaka ya kuwateua ni pamoja na Wakuu wa Mikoa.
“Binafsi sioni kama kunahaja ya kuwa na wakuu wa mikoa wala wakuu wa wilaya kwani hao wanaonekana kuwepo kwa ajili ya kujitengenezea ulaji tu.
“Lakini kazi kubwa inatakiwa ifanywe na Meya wa Jiji ambaye ni mchaguliwa wa wananchi kwa kupitia madiwani.”
Dk. Lwaitama anasema, “Inatakiwa tukubali kurudi katika Katiba ya Warioba ili kuondoa mfumo huu wa kuwa na viongozi wengi ndani ya mkoa mmoja.
“Tunatakiwa kubaki na Mkurugenzi wa Jiji na Meya wa jiji tu ambaye amebeba ndoto za wananchi na sio Mkuu wa Mkoa ambaye ameteuliwa tu.”
Habari hii kwahisani ya Mwanahalisi oline

MPINZANI ALIYESHINDA UWAKILISHI ZEC YAMTENGUA

Ofisa mdhamini wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Ali Mohammed Dadi amesema mshindi wa uwakilishi katika Jimbo la Ziwani ni Suleiman Ali wa CCM na si Asaa Hamad wa UPDP aliyetangazwa awali.

Dadi kutoka ofisi ndogo ya Pemba alisema jana kuwa msimamizi wa uchaguzi katika Wilaya ya Chakechake, Othman Hamisi alikosea wakati wa kujaza karatasi ya matokeo ya mshindi wa jimbo hilo.

“Nimezungumza naye na amesema kwamba alitoa ufafanuzi kuwa walifanya makosa katika kuandika matokeo, hivyo aliyeshinda ni mgombea wa CCM,” alisema.

Katika karatasi hiyo ya matokeo iliyokuwa imebandikwa ukutani, Asaa Ali Hamad alionekana kuwa amepata kura 221 dhidi ya 121 za mgombea wa CCM, lakini kwa ufafanuzi huo wa ZEC hakuna chama cha upinzani kilichoshinda nafasi ya uwakilishi au udiwani.

Kwa matokeo hayo, CCM imeshinda majimbo yote ya uwakilishi Unguja na Pemba na hivyo kuzidisha utata kwa Rais mteule, Dk Ali Mohamed Shein anayeapishwa leo, kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) kwa mujibu wa ibara ya 9 (3) ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 toleo la 2010.

Awali, kulikuwa na uwezekano wa UPDP kutoa mteule wa nafasi ya makamu wa kwanza wa Rais kwa kuwa kilitangazwa kimakosa kupata kiti cha uwakilishi baada ya CCM lakini baada ya ufafanuzi huo wa ZEC matumaini hayo yameyeyuka. 
 
Kuyeyuka kwa ndoto hiyo ya UPDP kunamaanisha kwamba hakuna chama kilichoshika nafasi ya pili kwa kupata kura asilimia 10 au zaidi, ambacho kwa mujibu wa Katiba hiyo kingekuwa na nafasi ya moja kwa moja kutoa makamu wa kwanza wa rais na baadaye mawaziri wa upinzani kuunda SUK. 
 
Tangu Dk Shein atangazwe kushinda urais katika uchaguzi wa marudio baada ya matokeo ya ule wa awali kufutwa, mjadala mkubwa kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii umekuwa ni jinsi gani atateua Serikali yake kukidhi matakwa ya Katiba ya kuwa na Serikali ya Umoja wa Kitaifa ili kuendeleza maridhiano ya kisiasa yaliyofikiwa baina ya CCM na CUF kabla ya uchaguzi wa 2010.

Wakati Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai akisema Rais Shein atatumia busara zake kumpata makamu wa kwanza wa rais, baadhi ya wanasheria wamesema hawaoni ufumbuzi wa moja kwa moja kutokana na upungufu huo wa kikatiba.

Kwa mujibu wa katiba ya Zanzibar, Rais atateua makamu wa kwanza wa Rais kutoka chama kilichoshika nafasi ya pili na mgombea wake wa urais kupata asilimia 10 ya kura za urais, au nafasi ya makamu wa kwanza itaenda kwa chama chochote cha upinzani kilichoshika nafaso pili kwa wingi wa viti vya majimbo katika Baraza la Wawakilish

Wednesday, March 23, 2016

MAALIMSEIF ASISITIZA CUF KUTOSHIRIKI UCHAGUZI WOWOTE CHINI YA........



SIKU mbili tangu kufanyika kwa uchaguzi wa marudio Zanzibar, na siku moja kabla ya kuapishwa Dk Ali Mohamed Shein, Maalim Seif Shariff Hamad, Mgombea wa Urais wa Zanzibar katika uchaguzi wa Oktoba 25 mwaka jana kupitia Chama cha Wananchi (CUF), amesema CUF haitashiriki uchaguzi wowote chini ya Tume ya Jecha Salim Jecha,

Akizungumza katika Hoteli ya Serena ambapo yupo kwa mapumziko baada ya kulazwa, Maalim Seif amesema kuwa kama yatatokea maridhiano yatakaoongozwa na kusimamiwa na taasisi huru za kidemokrasia, bila vitisho vya majeshi na polisi, kuwa na vyombo huru vya habari na tume huru sio hii iliyopo Zanzibar chini ya Jecha, hapo CUF kitaweza kufikiri kushiriki uchaguzi.

Ameongeza kuwa harakati za kudai haki, zitaendelea kwa njia ya amani ili marekebisho ya tume yafanyike kwani kwa utaratibu uliopo hata mwaka 2020 upinzani ukishinda Tanzania bara, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kitang’gang’ania madaraka.

“CUF tunaamini katika amani, tusichafue amani, tusichafue nchi yetu, tuendeleze mapambano kwa kutoitambua serikali iliyojiweka madarakani katika uchaguzi haramu wa Machi 20 mwaka huu, wala hatutaipatia ushirikiano wowote katika mambo yote” alisema.

Uchaguzi wa 20 Machi, sio halali. Jecha hakuwa na uwezo wa kisheria wala kikatiba kufuta uchaguzi, mgogoro uliopo sasa umesababishwa na Jecha, ukapewa baraka za CCM, sababu CCM hawataki kushindwa, na hawataki wapinzani kuongoza. Kila CCM ikishindwa hutoa visingizio.

“Kabla Kikwete (Rais Mstaafu Jakaya Kikwete) hajaondoka madarakani, aliniambia kuwa Maalim CCM wanakuogopa, wanajua ukishinda utaweza kuvunja Muungano, lakini nilimwambia, CCM ndio wenye jeshi, wenyewe ndio wenye dola mimi nitavunjaje Muungano?

Hiyo ni hofu na visingizio tu ili waendelee kukwapua madaraka.”Alisema.
Ameweka bayana kuwa kwa sasa CCM imewarejesha wananchi miaka 20 iliyopita, kwani uhasama wa watu kutengana kwenye shughuli za kijamii kwa sababu za tofauti za kisiasa zimeanza kurejea baada ya CCM kulazimisha kukwapua madaraka ya wananchi kwa kufuta uchaguzi wa 25 Oktoba mwaka jana.

Akizungumzia suala la Muungano kama ambavyo amekuwa akihusishwa Maalim seif amesema kuwa sasa Muungano utavunjwa na CCM, sio CUF wala yeye kama wanavyosingizia.

Ameongeza kuwa kwa sababu CCM ya bara ndio inalazimisha kuweka viongozi waliokataliwa na wananchi wa Zanzibar na chama chao kwa kutumia majeshi na polisi wao ndio husababisha wananchi wachukie Muungano.

Aidha kuhusu uchaguzi wa marudio wa Machi 20, Seif amesema kuwa CUF imeshinda, kwani wananchi wa Zanzibar waliitikia wito wa CUF, wakasusa, hawakujitokeza kupiga kura. Hizo zilizotangazwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) wanajua walipozipata wao na CCM.

“Mimi nilishasema tangu awali, kuwa matokeo yameshajulikana kabla ya uchaguzi, sababu ni ya kupika, namhurumia Dk Shein kwa kujisifu kupata kura ambazo hazipo, mawakala waliweka wao na wasimamizi na kuna taarifa kuwa wapigakura walikuwa wanapewa rundo la kura, wapige na kutumbukiza ili kukidhi matakwa ya CCM.” Amesema Maalim Seif.

Maalim Seif amewatakia utulivu Wazanzibar wote, na kuwaarifu kuwa afya yake ni imara, na atarejea Zanzibar wakati wowote kuungana nao.



Special thanks: Mwanahabari Huru (Jamii Forum)

Tuesday, March 22, 2016

BREAKING NEWS: UKAWA YABEBA UMEYA JIJI LA DAR

Baada ya vuta nikuvute nyingi kuhusu kiti hiki cha umeya Jiji la Dar mpaka kufikia hatua Rais Magufuli kuingilia kati kuwataka uchaguzi ufanyike hata kama CCM itaanguka. Hatimaye umefanyika leo hii na UKAWA wamenyakua Jiji hilo.

Mgombea wa UKAWA Issaya ameshinda Umeya wa Jiji muda mfupi uliopita kwa Kura 84 dhidi ya Kura 67 za Mgombea wa CCM  Yenga Omary. Madiwani watano wa CCM wameingia mitini hawakutokea kwenye uchaguzi licha ya CCM kukimbilia mahakamani mara kwa mara kuonesha wapo siriasi na kiti hiki.

SAKATA LA RUSHWA KAMATI ZA BUNGE ZITTO AJIUZULU



Kupitia ukurasa wake wa Facebook leo Asubuhi mbunge huyo wa Kigoma mjini Kabwe Zuberi Zitto aliandika yafuatayo kuonesha kujiuzulu kwake katika kamati anayohudumia
"Kuna tuhuma za rushwa dhidi ya Kamati mbalimbali za Bunge ikiwemo kamati ninayohudumu. Nimemwandikia Spika Kuomba Uchunguzi juu Ya tuhuma hizo na kwamba achukue hatua kali dhidi ya yeyote atakayekutwa kuhusika na vitendo vya rushwa. Nimejiuzulu Ujumbe wa Kamati ili Kutoa Nafasi Ya Uchunguzi Husika."

Mahakama Yatupilia Mbali Maombi ya Kuzuia Uchaguzi wa Meya wa Jiji la Dar Es Salaam


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imeamuru uchaguzi wa meya na naibu meya wa Jiji la Dar es Salaam, kufanyika leo kama ilivyopangwa.

Hakimu Mkazi Mkuu, Warialwande Lema alitoa uamuzi huo jana akijibu maombi yaliyokuwa yamewasilishwa na walalamikaji, Suzan Massawe na Saad Mohammed Kimji kupitia wakili wao, Elias Nawela dhidi ya Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam.

Wakati Mahakama ikitoa uamuzi huo, Rais John Magufuli amezitaka pande zinazogombea kiti cha umeya Dar es Salaam, kukamilisha mchakato huo katika uchaguzi uliopangwa kufanyika leo, badala ya kuendeleza malumbano.

Rais alitoa kauli hiyo jana Ikulu wakati akihakiki silaha zake. Alisema pande zote ziwe tayari kupokea matokeo ya uchaguzi huo, ili meya apatikane na jiji liweze kuendelea na mipango yake ya kuwahudumia wananchi bila vikwazo.

“Mahali tunapostahili kushinda kama tumeshinda tushinde kweli, lakini mahali tunaposhindwa napo tukubali kushindwa, hiyo ndiyo demokrasia ya kweli,” alisema Rais Magufuli.

Akitoa uamuzi wa Mahakama uliokuwa ukisubiriwa kwa hamu na walalamikaji na walalamikiwa, Hakimu Lema alisema Mahakama haikuona sababu za msingi kati ya zilizowasilishwa na walalamikaji kuishawishi kuzuia kufanyika kwa uchaguzi huo.

“Siyo busara kuendelea na sababu ambazo hazijathibitishwa,” alisema Hakimu Lema alipokuwa akitoa uamuzi huo na kuongeza kwamba kwa kukosekana orodha inayoonyesha majina ya wapigakura, haijulikani kama waleta maombi ni miongoni mwa wapigakura au la.

Hakimu Lema alisema walalamikaji hawakuwa makini tangu awali walipofungua shauri hilo, Februari 5 kwani hawakutokea mahakamani hadi Februari 14, wakili wao Nawela alipojitokeza na kuomba nakala ili awapelekee wajibu maombi jambo linalofanya washindwe kuishawishi Mahakama kuwapa haki yoyote kwa kuwa hawakufuatilia shauri lao tangu awali.

Mapema jana mchana, wakili Nawela aliiomba Mahakama itoe zuio la kufanyika uchaguzi huo na iamuru hali ibaki kama ilivyo hadi pale kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi kwa madai ya kwamba walalamikaji katika shauri hilo, hawajapewa haki yao ya kualikwa kushiriki katika uchaguzi huo.

Alidai kuwa iwapo uchaguzi huo utafanyika, basi maombi yao na kesi ya msingi yatakuwa hayana maana.

Akijibu hoja hizo, wakili Jumanne Mtinange kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, aliiomba Mahakama kuyaondoa maombi hayo kwa madai kuwa hayana msingi wowote.

Mtinange alidai hakuna uthibitisho wowote au orodha ya wapigakura kuonyesha kwamba waleta maombi wamekosekana, hivyo maombi ya kutaka hali ibaki kama ilivyo hayana uzito wowote.

Alisema maandalizi ya uchaguzi yana gharama na kwamba ni mara ya tatu umeahirishwa, hivyo kuomba uchaguzi wa leo uendelee kama kawaida.

Timu ya mawakili wa Chadema wakiongozwa na Wakili Peter Kibatala, Omary Msemo na John Mallya walikuwa muda wote wakifuatilia kesi hiyo mahakamani hapo.

Kwa uamuzi huo, kinyang’anyiro cha kugombea umeya sasa kimebaki kwa Isaya Mwita wa Chadema na Omary Yenga wa CCM wanaowania nafasi hiyo katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika leo katika Ukumbi wa Karimjee baada ya kuahirishwa mara tatu kwa sababu mbalimbali ikiwamo zuio batili la Mahakama kabla ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Tamisemi), George Simbachawene kuiagiza uchaguzi huo ufanyike kabla ya Machi 25.



Baadaye, Kaimu Mkurugenzi wa Jiji, Sarah Yohana alitangaza na kutoa barua kwa wajumbe husika juu ya wito wa kikao cha Baraza la Madiwani kitakachokuwa na ajenda ya uchaguzi akisema wajumbe 163 watashiriki kupiga kura, kati yao 87 ni kutoka Ukawa na 76 CCM.

(mpekuzi)

Monday, March 21, 2016

MWANAHABARI ALIYETEKWA AELEZA KILA KITU KUHUSU TUKIO HILO

SALMA Said, Mwandishi wa Habari wa Shirika la Utangazaji la Ujerumani (DW) pia Gazeti la Mwananchi amesema, licha ya kutekwa na kuteswa hatorudi nyuma, anaandika Regina Mkondo.

Amesema, kazi yake ya uandishi na kuripoti matukio mbalimbali ikiwa ni pamoja na yale yanayovunja haki za binadamu itaendelea kama kawaida.

Amesema hayo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam ikiwa ni siku mbili baada ya kutekwa na watu ambao hawakujitambulisha akiwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julisu Nyerere.

“Kupigwa kwangu sio kitu kikubwa zaidi ya kuzuiwa kuandika na kuripoti habari, sababu naamini wananchi walitarajia kusikia ripoti zangu na kufahamu hali halisi inayoendelea visiwani Zanzibar,” amesema Salma.

Amesema, wiki mbili kabla ya kufanyika uchaguzi wa marudio visiwani Zanzibar alipata ujumbe wa vitisho uliomtaka kujihadhari juu ya kazi anazozifanya za kuripoti taarifa ambazo ziliwakera baadhi ya viongozi.

“Kama mnavyojua tangu kufutwa matokeo ya uchaguzi mkuu wa Zanzibar Oktoba 25, 2015 kulitokea mambo mabaya katikati ikiwemo ukiukwaji wa haki za binadamu kama kupigwa, kutekwa na kutupwa nje ya mji,” amesema Salma na kuongeza;

“Sisi tunaoijua Zanzibar tunayaona haya, kuna baadhi ya mambo hayaripotiwi na vyombo vya habari kwasababu ya vyombo hivyo kupewa vitisho, lakini kwa waandishi wanaoripoti katika vyombo vya nje kama Aljazeera walifanikiwa kuandaa dokumentari ya matukio hayo.”

Salma amesema, watekaji hao walimwambia kuwa ametekwa ili kuzuiwa kutoendelea kuripoti habari za uchaguzi.
“Awali nilipigiwa simu na kutumiwa ujumbe wa simu wa kunionya, nilikuwa nafuatwa hadi ofisini kwangu, kuna siku nilifukuzwa na gari hadi nikadondoka chini,” amesema.
“Nimeteswa kwasbabau ya kazi zangu za kutaka kutetea wananchi wenzangu na nchi yangu, kuna siku nilihoji juu ya fedha kiasi cha biloni 7 zilizotumika kwa ajili ya uchaguzi wa marudio, nahisi iliwakera baadhi ya watawala,” amesema.
Salma amewataka waandishi wa habari kuacha kuandika habari za kufurahisha baadhi ya watu huku wakiumiza wananchi bali waandike habari ambazo zinaeleza matatizo ya jamii.
“Kama mwandishi ni jukumu langu la kuhakikisha kuwa natoa msaada kwa jamii kupitia taaluma yangu, nchi yetu ina matatizo mengi yanayohitaji kuripotiwa ili viongozi wayajue na kuyatatua,” amesema.
Amewataka waandishi wa habari kuwa na umoja na kuacha kuwakashfu baadhi ya waandishi wanaopata shida kama alizopata yeye.

credit: Fullhabari

Friday, March 18, 2016

KUELEKEA UCHAGUZI Z'BAR WABUNGE WA CUF WACHAFULIWA WAZUSHIWA

Andiko hilo limesambazwa katika mitandao mbalimbali lakini CUF wamekanusha si kauli yao na kuwataka wananchi walipuuze. 
Kupitia ukurasa wake wa Facebook Ismail Jussa ameandika "Kuna kitu hichi kinasambazwa kikidaiwa kwamba ati ni barua ya Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Mhe. Nassor Ahmed Mazrui (ambapo waliotunga wamemuandika ni Ahmed Nassor Mazrui).
Hakuna kitu kama hicho. Tunawaomba wananchi wote WAKIPUUZE!"
 

Thursday, March 17, 2016

CHADEMA WAMSHUTUMU RAIS MAGUFULI KWA VISASI

RAIS John Magufuli anatajwa kuwa mtawala anayeendekeza kisasi cha kiutawala kwa wananchi walioamua kupigia kura vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), anaandika Regina Mkonde.

Jana wakati Rais Magufuli akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa kituo cha kufua umeme cha Kinyerezi namba mbili alisema, “huwezi ukapeleka chakula kwa mtoto wa jirani” kauli ambayo imeeleza kuwa ya kibaguzi.

Kauli hiyo imetafsiriwa na Ukawa kwamba Rais Magufuli anaonekana kutokuwa tayari kushirikiana na vyama hivyo (jirani) licha ya kuwa ndio walio wengi katika kuwawakilisha wananchi jijini Dar es Salaam.

Kauli hiyo pia imejadiliwa kwa upana kwenye mitandao ya kijamii kutokana na kuwa na ukakasi uliotoa tafsiri mbalimbali.

Charles Kuyeko, Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala amesema, kauli hiyo imelenga kuwaponda viongozi wa upinzani na kwamba, inaleta picha mbaya katika ulimwengu wa demokrasia nchini.

“Kauli yake imelenga kuuponda upinzani, licha ya hayo kampeni zimeisha, hakuwa na sababu ya kuongea kauli hiyo mbele ya wananchi katika shughuli za kitaifa ambazo hazilengi itikadi za kisiasa,” amesema Kuyeko.

Amesema kuwa, huu si wakati wa kujadili tofauti za itikadi za vyama bali ni wakati wa kutatua changamoto za wananchi.

Boniface Jacob, Meya wa Manispaa ya Kinondoni amesema kuwa, hata kama rais ataitekeleza kauli yake, haitaathiri maendeleo ya halmashauri yake kwasababu mapato yake yanakidhi mahitaji yake.

“Kwa upande wangu kauli yake haitaniathiri kwasababu Kinondoni tunajiweza hatutegemei sana msaada kutoka serikali kuu. Kinondoni ina uwezo wa kukusanya mapato ya kiasi cha bilioni 50 kwa mwaka,” amesema Jacob.

Amesema, Kinondoni ina vyanzo vingi vya mapato, ambapo mapato yake yanatosha kutekeleza ahadi zake ikiwemo uboreshaji wa miundombinu na huduma za kijamii.

“Hata kama atajaribu kutuwekea vikwazo ili tushindwe tekeleza ahadi zetu na kuonekana hatufai mbele ya wananchi, hatofanikiwa, tutatekeleza ahadi zetu na wananchi watashuhudia mabadiliko ya uongozi wa UKAWA.

Pia amenukuliwa akisema, “nawapongeza wakazi wa Kinyerezi kwa kunichagulia mbunge anayetoka kwenye chama changu, nawahakikishieni kama kuna changamoto za Jimbo la Segerea nitazipa kipaumbele katika utatuzi wake.”

Licha ya hayo, Magufuli amesema aliamua kumchagua Paulo Makonda aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa lengo la kuwanyamazisha maadui zake.
“Hata Makonda nimemuacha Dar es Salaam ili wabaya wake wamuone akipanda cheo, wenye chuki wajinyonge zaidi,” amenukuliwa Rais Magufuli

WAZIRI WA MAGUFULI AUMBULIWA NA CUF KWA KUSEMA UONGO KUHUSU Z'Bar


Naibu Katibu Mkuu wa CUF (Bara) , Magdalena Sakaya akionyesha picha ya mhanga wa vipigo zanzibar.

WAKATI uchaguzi wa marudio ukitarajiwa kufanyika jumapili visiwani Zanzibar, Chama Cha Wananchi (CUF) kimesema kuwa haki za binadamu zimeendelea kuminywa kwa kiasi kikubwa visiwani humo huku wafuasi wa chama hicho wakilengwa zaidi.

Naibu Katibu Mkuu wa CUF (Bara) , Magdalena Sakaya, ameyasema hayo leo wakati alipozungumza na waandishi wa habari kwenye Makao Makuu ya Ofisi za Chama hicho zilizopo Buguruni  jijini hapa.

Magdalena amesema kuwa Tanzania imeridhia mikataba mbalimbali ya kimataifa ya haki za binadamu hivyo mambo yanayotokea Zanzibar ni ya kushangaza na hayapaswi kufumbiwa macho kwa ustawi wa Taifa.

Amesema kuwa baada ya CUF kutangaza kujitoa kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi wa marudio , wananchi wa Zanzibar wamekuwa wakiishi kwa hofu huku vikundi vya matukio ya uhalifu maarufu’mazombi’ yakipiga watu pasipo na kuchukuliwa hatua zozote na vyombo vya usalama.

“Mara kwa mara tumekuwa tukiwaambia jeshi la polisi kuhusiana na haya mazombi ila cha kushangaza hadi leo hakuna taarifa yoyote iliyotolewa kuhusiana na kukamatwa kwa makundi hayo ya mazombi,”alisema.

Chama hicho kimesema kuwa viongozi wao kadhaa wamekamatwa kwa nyakati tofauti ambapo jana Mkurugenzi wa Habari na Uenezi Taifa -Hamad Masoud, alikamatwa na kuwekwa kizuizini na Polisi baada ya kutoa taarifa ya matukio mbalimbali yanayoendelea visiwani humo ambayo ni ya kinyume na haki za binadamu.

“Jambo la kushangaza kila tukio baya likitokea wanasingiziwa wafuasi wetu, mara kwa mara wamekuwa wakikamatwa na tangu januari hadi sasa zaidi ya wafuasi 60 wamekamatwa kwa madai ya kuhusika na uvunjifu wa amani,”alisema.

“Sisi tumeamua kujitoa kwenye uchaguzi huo ili wananchi wetu wawe huru na kuwaepusha kwenye vurugu, kwa hiyo
Chama cha Mapinduzi kisiwalazishe wananchi kufanya mambo ambayo wenyewe hawako tayari kuyafanya na kuyaona ni kinyume na Katiba, kwa sababu uchaguzi huo wa marudio ni haramu.



“Asilazimishwe mbuzi kunywa maji wakati hana kiu,”alisema Magdalena na kuongeza kuwa wangetegemea uchaguzi huo kufanyika kwa amani baada ya kutangaza kujitoa mapema mwaka huu.


Magdalena alisema kuwa yapo maeneo kadhaa visiwani humo wananchi wamepigwa marufuku ya kutoonekana wakitembea kuanzia saa mbili usiku hatua inayosababisha hata wengine kushindwa kwenda kufanya ibada.

Akizungumzi kauli ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga, ya kusema kuwa hakuna watu wanaopigwa visiwani humo, Kiongozi huyo wa Chama alipinga madai hayo na kusema kuwa ni hatari kuudanganya umma kwa kuficha ukweli na kuacha watanzania wateswe.

Aliishauri Serikali kuhakikisha kuwa usalama wa wananchi visiwani humo unaimarishwa kwa kufuata misngi ya haki za binadamu na utawala bora, pia ichukue hatua dhidi ya ‘mazombi’ ambayo yamekuwa yakiripotiwa kupiga watu kwa nyakati tofauti. 


credit: FULLHABARI

 

Top