Games

LATEST UPDATES

Saturday, February 2, 2013

MTWARA WAMBANA PINDA, WAMPINGA


Moja ya picha ya tukio la Maandamano zidi ya madai ya Kupinga gesi kuitoka Mtwara kwa bomba hadi Dar es Salaam

LICHA ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kufichua siri akiwa Dodoma kuwa amebaini kuwa kuna mpasuko mkubwa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), mkoani Mtwara na harakati za kisiasa ni sababu zilizochochea mgogoro huo wa madai ya gesi, baadhi ya wananchi mkoani hapa bado hawajaridhika hivyo wameyakataa maelezo yake.

Baadhi ya wananchi waliomsikiliza waziri mkuu walisema hawakubaliani na maelezo yake na Taasisi ya Shura ya Maimamu Mtwara imesema kwamba haijaridhishwa na majibu yasiyo na mashiko ya Pinda katika hoja nzito na kwamba bado serikali haijaupatia suluhu mgogoro huo.

“Wana Mtwara tunahitaji ‘powerplant’, mashine za kufua umeme pamoja na hiyo ya kuchakata gesi iwe Mtwara… katika eneo hilo hatujaridhika,” msemaji wa shura hiyo, Sheikh Abubakar Mbuki alisema.

“Waziri Mkuu asituambie tu gharama za kutandaza nyaya ni kubwa kuliko bomba la gesi akaishia hapo. Atuambie gharama hizo ni kiasi gani? Mbona gharama za bomba zipo wazi, kwa nini hizi za nyaya hazisemwi?” alihoji Sheikh Mbuki.

Naye Mwenyekiti wa Vijana wa Chama cha Wananchi (CUF) Taifa, Katani Katani alikuwa na haya ya kusema: “Tunachokataa sisi wana Mtwara ni kusafirisha gesi kwa njia ya bomba, tunataka mashine zinazojengwa Kinyerezi zihamishiwe Mtwara.”

Alisema kutokana na kutopatikana kwa ufumbuzi wa madai hayo, bado wananchi wa Mtwara wataendelea kupinga mradi huo na hali itakuwa tete.

Share This :

Post a Comment

 

Top