Games

LATEST UPDATES

Monday, March 21, 2016

MWANAHABARI ALIYETEKWA AELEZA KILA KITU KUHUSU TUKIO HILO

SALMA Said, Mwandishi wa Habari wa Shirika la Utangazaji la Ujerumani (DW) pia Gazeti la Mwananchi amesema, licha ya kutekwa na kuteswa hatorudi nyuma, anaandika Regina Mkondo.

Amesema, kazi yake ya uandishi na kuripoti matukio mbalimbali ikiwa ni pamoja na yale yanayovunja haki za binadamu itaendelea kama kawaida.

Amesema hayo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam ikiwa ni siku mbili baada ya kutekwa na watu ambao hawakujitambulisha akiwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julisu Nyerere.

“Kupigwa kwangu sio kitu kikubwa zaidi ya kuzuiwa kuandika na kuripoti habari, sababu naamini wananchi walitarajia kusikia ripoti zangu na kufahamu hali halisi inayoendelea visiwani Zanzibar,” amesema Salma.

Amesema, wiki mbili kabla ya kufanyika uchaguzi wa marudio visiwani Zanzibar alipata ujumbe wa vitisho uliomtaka kujihadhari juu ya kazi anazozifanya za kuripoti taarifa ambazo ziliwakera baadhi ya viongozi.

“Kama mnavyojua tangu kufutwa matokeo ya uchaguzi mkuu wa Zanzibar Oktoba 25, 2015 kulitokea mambo mabaya katikati ikiwemo ukiukwaji wa haki za binadamu kama kupigwa, kutekwa na kutupwa nje ya mji,” amesema Salma na kuongeza;

“Sisi tunaoijua Zanzibar tunayaona haya, kuna baadhi ya mambo hayaripotiwi na vyombo vya habari kwasababu ya vyombo hivyo kupewa vitisho, lakini kwa waandishi wanaoripoti katika vyombo vya nje kama Aljazeera walifanikiwa kuandaa dokumentari ya matukio hayo.”

Salma amesema, watekaji hao walimwambia kuwa ametekwa ili kuzuiwa kutoendelea kuripoti habari za uchaguzi.
“Awali nilipigiwa simu na kutumiwa ujumbe wa simu wa kunionya, nilikuwa nafuatwa hadi ofisini kwangu, kuna siku nilifukuzwa na gari hadi nikadondoka chini,” amesema.
“Nimeteswa kwasbabau ya kazi zangu za kutaka kutetea wananchi wenzangu na nchi yangu, kuna siku nilihoji juu ya fedha kiasi cha biloni 7 zilizotumika kwa ajili ya uchaguzi wa marudio, nahisi iliwakera baadhi ya watawala,” amesema.
Salma amewataka waandishi wa habari kuacha kuandika habari za kufurahisha baadhi ya watu huku wakiumiza wananchi bali waandike habari ambazo zinaeleza matatizo ya jamii.
“Kama mwandishi ni jukumu langu la kuhakikisha kuwa natoa msaada kwa jamii kupitia taaluma yangu, nchi yetu ina matatizo mengi yanayohitaji kuripotiwa ili viongozi wayajue na kuyatatua,” amesema.
Amewataka waandishi wa habari kuwa na umoja na kuacha kuwakashfu baadhi ya waandishi wanaopata shida kama alizopata yeye.

credit: Fullhabari
Share This :

Post a Comment

 

Top